Burundi : tume ya haki za binadamu imethibitisha kukamatwa kwa Bunyoni

Burundi : tume ya haki za binadamu imethibitisha kukamatwa kwa Bunyoni

Tume huru ya kitaifa ya haki za binadamu (CNIDH) imetangaza hayo kupitia ukurasa wake wa Twitter. Sixte Vigny Nimuraba kiongozi wa tume hiyo alihakikishia SOS Médias Burundi kuwa amemuona aliyekuwa waziri mkuu Alain Guillaume Bunyoni katika eneo anakozuwiliwa bila hata hivyo kusema eneo ambako anazuwiliwa jemedali huyo wa polisi. HABARI SOS Médias Burundi

Kwenye ukurasa wake wa Twitter, CNIDH imeandika jumamosi hii mchana kuwa imeona jemedali wa polisi Alain Guillaume Bunyoni katika eneo anakozuiliwa bila kutaja eneo lenyewe. Lakini inahakikisha kuwa hakufanyiwa kisa chochote cha mateso.

” Tumefanya kazi yetu na familia imepewa taarifa. Kinachosalia, ni huduma zenye mamlaka kutangaza”, amejibu Bwana Nimuraba wakati SOS Médias Burundi ilipomuuliza eneo anakozuiliwa Bunyoni.

” Hakuna mtu mwingine aliyekamatwa akiwa pamoja na waziri mkuu wa zamani” amefahamisha Sixte Vigny Nimuraba, kiongozi wa tume ya CNIDH.

Hadi sasa, hakuna taasisi yoyote ya serikali iliyotoa tangazo kuhusu kukamatwa kwa mmoja kati ya majemedari wenye ushawishi na utajiri mkubwa kutoka kundi la waasi la zamani la kabila la wahutu, chama cha CNDD-FDD kinachotawala kwa wakati huu tangu 2005 kutokana na mkataba wa Arusha ( Tanzania) wa amani na maridhiano wa mwaka 2000.

Lakini mtoto wake mkubwa wa kike Darlene Bunyoni akiwa nje ya nchini Burundi, siku ya ijumaa aliandika kwenye ukurasa wake wa Twitter kuwa baba yake anazuiliwa na idara ya ujasusi na kuzidi kuwa ana wasi wasi kuhusu usalama wake, na kuomba sheria ichukuwe mkondo wake.

Mwanaharaki ambaye anaishi uhamishoni Pacifique Nininahazwe, alisema kuwa waziri mkuu huyo wa zamani alikamatwa akiwa katika eneo la Bujumbura ( magharibi mwa Burundi).

Jumatano, waziri wa Burundi wa mambo ya ndani na usalama Martin Niteretse aliyethibitisha kuwa jemedari huyo wa polisi hapatikani na kwamba anatafutwa na korti kuu ya jamuhuri.

Mwendeshamashtaka mkuu wa jamuhuri Sylvestre Nyandwi pamoja na msemaji wake Agnes Bangiricenge hawakupatikana ili kujibu maswali yetu. Lakini mwendeshamashtaka mkuu huyo aliamuru ufanyike msako kwenye makaazi mawili ya waziri mkuu huyo wa zamani katika jiji la Bujumbura na mkoani Rutana. Matokeo ya msako huo hayakutangazwa lakini mkoani Rutana vyanzo vya polisi viliambia SOS Médias Burundi kuwa hapakuwa kitu katika nyumba hiyo iliyojengwa kwenye ardhi kubwa vikiwemo viwanja vya michezo na ofisi ndani yake.

” Hata kabati la cuma lililokuwa ndani ya chumba chake, lilikuwa tupu” waliambia SOS Médias Burundi askali polisi vyanzo vyetu.

Kwenye waranti wa kutoa ruhsa ya kufanya msako huo katika makaazi ya Bunyoni, mwendeshamashtaka aliandika kuwa ” huenda ndani ya makaazi hayo kuna kitita kikubwa cha pesa kilichofichwa ndani ya makaazi hayo”.

” Itakuwa vigumu kupata ushahidi wa tuhuma dhidi ya Bunyoni iwapo watataka kuonyesha kuwa alipata utajiri katika njia haramu au alihusika na kuhujumu uchumi sababu kabla ya kuingia madarakani, hakuonyesha mamlaka mali zake na wakati alipofutwa kazi, mali zake pia hazikuonyeshwa. Na wakati vyombo vya habari vilipomutuhumu kujihusisha na visa vya rushwa , hakuna uchunguzi uliofunguliwa dhidi yake ” anadai mwakilishi mmoja wa shirika la kiraia la ndani.

Afisa huyo wa polisi ya Burundi mwenye cheo kikubwa kuliko wote cha jemedali kamishena wa polisi sawa na jemedali wa jeshi alikuwa afisa wa kwanza kutoka kundi la zamani la waasi wa kihutu kuingia rasmi katika polisi ya taifa (PNB), analengwa na vikwazo vya marekani. Nchi hiyo yenye nguvu duniani iliwahi kuondoa vikwazo dhidi yake katika mwaka wa 2020 alipoingia madarakani na kuvirejesha badaye mwezi disemba 2022 miezi mitatu baada ya kufutwa kazi.

Anatuhumiwa kuhusika na visa vya maovu na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu katika nchi hiyo ndogo ya afrika mashariki.

Hakuna taasisi ya kisheria ambayo hadi sasa tayari ilifungua uchunguzi dhidi ya muwasi huyo wa zamani ambaye ni nadra kwake kuzungumzia maswala ya siasa. Bunyoni anatuhumiwa pia kumiliki makampuni mengi ya uchimbaji wa madini mashariki mwa nchi kubwa ya Afrika ya kati- Kongo na kuwa na ushirikiano wa kibiashara na rais mstaafu wa Tanzania Jakaya Kikwete.

Previous Kakuma (Kenya) : maradhi ya usafi mdogo yatishia waomba hifadhi
Next Kuhusu-Bunyoni: mahakama kuu imeanza uchunguzi dhidi ya Bunyoni