Burundi : noti mpya za elfu tano na elfu kumi zawekwa katika mzunguko wa pesa
Benki kuu ya Burundi (BRB) ilifamisha kuwa imeweka katika mzunguko wa pesa nchini Burundi noti mpya za elfu tano na elfu kumi kurejelea zile zilizotengenezwa tangu mwaka wa 2018. Gavana wa benki kuu ya Burundi BRB alisema hatua hiyo ilichukuliwa baada ya kugundua ongezeko la mzunguko wa noti hizo katika hali isiokuwa rasmi na hivyo kusababisha uzorotaji wa shughuli za mashirika ya fedha. HABARI SOS Médias Burundi
Hatua hiyo ilitangazwa jumatano mchana . Gavana wa BRB kupitia tamko rasmi alifahamisha kuwa uhaba wa noti za elfu tano na elfu kumi unashuhudiwa katika hazina za benki na mifuko ya fedha na kuvuruga shughuli za kulipa na kutuma pesa.
Katika kikao na wandishi wa habari, Dieudonné Murengerantwari alisema kuwa noti hizo mbili zinazolengwa ( elfu 5 na elfu 10 sarafu ya Burundi) zilizotengenezwa tarehe 4 julai 2018 zitaondolewa katika mzunguko wa sarafu kuanzia tarehe 17 juni 2023″.
Aliongeza kuwa muda wa siku kumi ulipewa wamiliki wa noti hizo ili wawe wameziweka kwenye akaunti zao. Kwa wale wasiokuwa na akaunti, ni lazima wafungue akantu kwa ajili ya kuheshimu muda huo uliyotolewa.
Ni budi kusisitiza kuwa kwenye akaunti ya mtu binafsi, hakuna kuzidisha kitita cha milioni kumi sarafu za Burundi , huku kwenye akaunti ya kampuni au shirika ikiruhusiwa kuweka milioni 30 kila siku na kwa kila akaunti.
Katika kikao hicho na wandishi wa habari, mkuu wa benki kuu ya taifa alifahamisha kuwa atawatuma wafanyakazi wa benki kuu ili kuwasaidia watu wanaoishi vijijini mbali na vituo vya mauzo.
Benki kuu ya taifa BRB ilifamisha kuwa noti hizo mpya za elfu kumi na elfu tano zilizotengenezwa tarehe 7 novemba 2022 zimewekwa rasmi katika mzunguko wa pesa .
Mtazamo wa baadhi ni kwamba BRB imetekeleza mpango wa rais wa jamuhuri ya Burundi. Hivi karibuni, rais wa Burundi alitishia watu wanaoweka vitita vikubwa vya pesa katika majumba yao kwamba siku moja watajikuta noti hizo zikiwa zimegeuka kama karatasi za kawaida.
Alhamisi, msemaji wa waziri wa mambo ya ndani na usalama alitoa wito kwa magavana wa mikoa ” kuwahamasisha wananchi wanaoishi katika maeneo ya mbali ili kila mtu afahamu kuhusu hatua hiyo ya benki kuu ya taifa”.